Wizara ya Utamaduni Sanaa na Michezo imewasilisha malalamiko rasmi kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na kuwataka klabu ya Yanga kugharamia uharibifu uliofanyika uwanja wa Benjamin Mkapa kwenye mchezo wao dhidi ya Al Ahly .

Kupitia barua hiyo, Wizara imekemea vikali kitendo hicho kilichotokea na kuutaka uongozi wa klabu ya Yanga kuwasiliana na uongozi wa uwanja ili kubaini ukubwa wa uharibifu huo. Barua ya Wizara inasema ,

Wizara ilitoa kibali cha kufanyika kwa mchezo wa kimataifa kati ya Yanga SC (Tanzania) dhidi ya Al-Ahly (Misri) katika Uwanja wa Benjamin Mkapa uliofanyika tarehe 2 Desemba, 2023 majira ya Jioni.

Hata hivyo, Wizara imepokea malalamiko kutoka kwa Uongozi wa Uwanja ambapo mashabiki wa Klabu ya Yanga wanalalamikiwa kwa kuwasha fataki wakati mchezo ukiendelea na kusababisha vurugu zilizopelekea baadhi ya viti kung’olewa.

Wizara inakemea vikali kitendo hiki na kuwataka Klabu ya Yanga mara moja kuwasiliana na Uongozi wa Uwanja ili kuweza kubaini ukubwa wa tatizo na kuona namna bora ya kulitatua.

Kwa barua hii, Wizara inawasilisha rasmi malalamiko haya kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kwa kuwa ndiye mdhamini wa vilabu hivi kwa maombi ya matumizi ya Uwanja huu ili kuwajulisha Klabu ya Yanga SC kuwa inapaswa kugharamia matengenezo ya viti vilivyong’olewa na Mashabiki wakati wa mchezo huu.

Aidha kuwaonya mashabiki wao kuacha mara moja tabia hizi ili uendelea kustawisha michezo
na kuulinda Uwanja wa Benjamin Mkapa.

Maoni yako ni yapi baada ya kusoma kile ambacho Wizara imeweza kukitoa? Usisahau kusoma zaidi taarifa zetu hapa.

1 Comment

  1. Pingback: Kombe La Dunia Kwa Vilabu Kuanza Kesho Saudi Arabia - Kijiweni

Leave A Reply


Exit mobile version