Huenda hii ndio vita yenye mvuto zaidi inayosubiriwa kati ya Feisal Salum ‘Fei Toto’ wa Azam FC na Stephane Aziz Ki wa Yanga ambao wote hadi sasa wanawania Tuzo ya Ufungaji Bora kutokana na kila mmoja wao hadi sasa kufunga mabao 18.

Yanga inakamilisha ratiba dhidi ya Tanzania Prisons kwenye Uwanja wa Azam Complex lakini akili zao zote ni kwa Aziz kuhakikisha anatwaa Kiatu cha Dhahabu Dar es Salaam. Lakini Azam FC ikiwa ugenini kucheza na Geita Gold nayo ina vita ya kuwania nafasi sambamba na kiatu cha Fei.

Katika mabao yake 18, Aziz Ki amefunga matatu kwa penalti huku Fei Toto akiwa ana bao moja tu la penalti, jambo linaloweza kumpa faida zaidi ikiwa watalingana idadi ya mabao baada ya mechi za mwisho leo kutokana na kanuni za Ligi Kuu Bara msimu huu kwenye vita ya ufungaji bora ilivyo.

Iko hivi, kanuni ya (13:1) kuhusu mshindi wa Tuzo ya Mfungaji Bora inaeleza, ikiwa wachezaji zaidi ya mmoja wamefungana idadi ya mabao njia ya kwanza itakayotumika wataangalia mabao yaliyofungwa kwa njia ya kawaida yatapewa alama mbili (2).

Mabao yatakayofungwa kwa njia ya penalti yatapewa alama moja (1) na ikiwa watalingana pia itatumika kanuni ya (13:2) inayoelezea mchezaji aliyecheza dakika chache atakuwa mshindi na ikitokea wakalingana pia itaangaliwa kanuni ya (13:3).

Kanuni hiyo ya (13:3) inaeleza, kama vigezo vyote vilivyowekwa vinafanana pia basi, nyota aliyefunga mabao mengi ugenini atakuwa mshindi.

Ieleweke wazi kwamba, mpaka sasa takwimu zinaonyesha kuwa Fei Toto amecheza mechi 28 kwa dakika 2,352, wakati Aziz Ki akiwa na dakika 1,994 katika mechi 25.

Mbali na kutaka kuibuka tu kidedea ila kila mchezaji anaweza kujitengeneza rekodi yake kwani endapo Feisal atafunga bao angalau moja tu ataifikia rekodi ya mabao 19 iliyowekwa na aliyekuwa nyota wa Azam FC, John Bocco msimu wa 2011/2012 ya kuwa mchezaji wa timu hiyo aliyefunga mabao mengi zaidi katika msimu mmoja wa Ligi Kuu.

Kwa upande wa Aziz Ki licha ya kuwania tuzo hiyo ila wengi wanaangalia ni vipi anaweza kuifikia au kuivunja rekodi ya aliyekuwa mshambuliaji wa kikosi hicho, Amissi Tambwe aliyefunga mabao 21 ndani ya msimu mmoja aliyoiweka 2015/2016.

SOMA ZAIDI: Funga Kazi Ligi Kuu Iko Hivi | Vita Ya Nafasi Ya Pili Na Kiatu

16 Comments

Leave A Reply


Exit mobile version