Ilipoishia Usijali Jacklin nipo kwa ajili yako mara zote” alisema  Mosses na kunifanya nitabasamu kwa uchovu, shughuli ilikuwa  pevu na vile nimetoka kuumwa basi nilichoka sana nikalala  palepale. 

Osman alipofika ofisini alihitaji kuniona ila aliambiwa kuwa  nimetoka, akiwa kama Bosi wangu alihitaji kujuwa niko wapi,  alinipigia sana simu lakini haikupokelewa maana nilikuwa  nimelala chakali, basi alipiga kwa Mama na kumuuliza kama  nitakuwa nimeenda nyumbani, Mama alimwambia Osman kuwa sipo  nyumbani. Endelea

SEHEMU YA TANO

“Haya Mama nitaendelea kumtafuta” Alisema Osman, alipokata  simu alijiuliza nilikuwa nimeenda wapi, alishikwa na wivu  fulani hata kazi hakufanya naye aliondoka. Mida ya Jioni kama  saa moja kasoro hivi ndiyo niliamka, nilikuta Mosses  ameniandalia supu, nilikunywa kisha aliniuliza 

“Osman ndiyo Nani? Amepiga sana simu, ilipokata yake iliingia  ya Mama yako, walikuwa wakipiga kwa kupokezana” Aliniuliza na  kuelezea kuhusu simu zilizokuwa zimeingia 

“Osman ni Bosi wangu labda amenipigia sababu kuna faili zipo  kwangu, ngoja nimpigie Mama” Nilisema, alinisogezea simu mara  moja kisha nilimpigia Mama, alipokea na kinishushia swali juu 

“Jacklin uko wapi?” Aliuliza kwa sauti iliyoonesha kuwa  alikuwa na shahuku ya kujuwa nilipo 

“Mama mimi siyo Mtoto sasa swali gani hilo alafu kama vile  una hasira na Mimi!” 

“Ndiyo wewe siyo Mtoto lakini kwanini uondoke kazini kabla ya  muda wa kazi kuisha? Osman amenipigia simu kujuwa kama upo  sawa na upo wapi” 

“Ulimjibuje Mama” 

“Nilimwambia kuwa sijui ulipo sasa kwanini niwe muongo kwa  kijana wa Watu, mwisho wote tuje kuonekana hatuna maana?” 

“Ok Mama usiongee sana nipo kwa Mosses hata hivyo narudi muda  siyo mrefu” Nilisema, Mama alikata simu. 

“Huyo Mama yako jinsi anavyonichukia usikute amekasirika huko  kisa wewe kuja kwangu” Alisema Mosses 

“Ah! Mama yangu nimeshamzoea love, ngoja nirudi tu nyumbani  ila fanya kama tulivyoongea tafuta nyumba kesho unipe jibu”  Nilisema kisha nilizama kwenye waleti yangu nikampa Mosses  laki na nusu 

“Hiyo itakusaidia” Nilisema kisha niliondoka zangu pale. 

Nilipofika nyumbani nilimkuta Mama akiwa amefura kama chura  mwenye njaa, alikuwa amekaa nje akinisubiria. Nilipomfikia  aliniuliza swali gumu sana 

“Umesahau kila kitu sababu leo upo hai, huyo Mosses alikataa  kusaidia Maisha yako, alinijibu jeuri lakini wewe unamuona wa  maana sana kwako, nimefanya makosa kukupigania Jacklin?” 

Lilikuwa ni swali gumu kuwahi kuulizwa katika Maisha yangu,  Mama alidondosha chozi lililochuruzika hadi kwenye mashavu  yake, ilinibidi nikae kwanza 

“Mama ndiyo maneno gani hayo? Binadamu tunakosea na  kujirekebisha, usimuhukumu Mosses kwa kosa moja tu yule ni  Binadamu hajakamilika Mama, hilo haliwezi kuuondoa uthamani  wake kwangu” Nilimjibu Mama kwa kujikaza sana, hakuna kitu  nilikuwa sipendi kama kumuona Mama akilia kwa ajili yangu,  anagalau ningekuwa mgonjwa lakini ni mzima na analia kwa  ajili yangu 

“Mama yako nilisemewa vibaya, Kijana wa Watu alikusaidia  hakuangalia nyuma. Bila Osman ingekuwa inasimuliwa hadithi  yako Jacklin, lakini leo Mtu aliyekusaidia akabadilisha na  Maisha yetu kututoa kwenye umasikini hadi kwenye hali hii  haupokei simu zake, unaacha kazi yake na kwenda kwa Mosses?”  Alisema Mama, nilihema kwa uchungu na maumivu, ni kweli Osman  alisaidia Maisha yangu lakini hakusaidia ili niwe mtumwa  kwake 

“Mama msaada ambao unakuwa Mtumwa ni msaada wa kizandiki tuu,  kama alinisaidia kwa moyo wake hakupaswa kuhitaji malipo,  mbona anajuwa kila kitu sasa kwanini apige simu kwako?  Amenikosea sana” 

“Unajisikiliza Jacklin au unaongea kwasababu unayo nafasi ya  kufanya hivyo? Hajakusaidia tu bali ameweka maisha yake  rehani, anatembea na figo moja kwa ajili yako, hupaswi  kumsumbua hivi kijana wa Watu na kama huitaji kazi basi  mwambie ili amtafute Mtu mwingine” Mama alisema kwa hisia  kali 

“Sawa Mama sipendi ukwazike kwa ajili yangu. Nitamuomba  msamaha Osman, kuwa na amani Mama nakupenda sana” Nilisema  kisha nilinyanyuka na kuingia ndani, nilimuacha Mama akiwa  amekaa nje peke yake, najuwa jinsi alivyokuwa anajisikia ila  ningefanya nini wakati moyo wangu upo kwa mwingine? Niliziona  ishara zote kuwa Osman ananipenda ila tayari hisia zangu zipo  kwa Mosses. 

Nilipofika chumbani kwangu niliyatafakari maneno ya Mama  ambayo ni wazi aliyasema kutoka ndani ya nafsi yake,  nilijisikia vibaya, nilitamani kumtumia meseji Osman nimuombe  msamaha ila niliona ni bora nimuombe msamaha kesho yake  Ofisini, nilizitazama Missed Calls zake nilimuonea huruma  Kijana wa Watu, nilifunua shati langu nikaangalia eneo la  tumbo, nilitabasamu tu hata sijui kwanini nilifanya hivyo.

Kesho yake kabla ya kwenda ofisini nilipitia duka la Maua  nikanunua ua zuri kwa ajili ya kumpatia Osman ili anisamehe  kwa kilichotokea. Nilichagua ua zuri ambalo niliamini litampa  furaha Osman, mvua zilikuwa zinaendelea kunyesha, hali ya  hewa ilikuwa nzuri sana ikanikumbusha siku ya kwanza  Nilipoanza kuumwa nikasaidiwa na Osman, nilianza kutabasamu  tu hadi Muuza Maua alinishtukia akasema 

“Inaelekea unampenda sana Mtu ambaye unampelekea ua hili,  Nawaombea penzi lenu lichipue mithiri ya Mtende jangwani”  Alisema kisha alinitazama usoni, ghafla sura yangu ilikosa  uchangamfu. Sijui kwanini kila nilipomfikiria Osman  nilijikuta nikiishia kwenye huzuni. Mara muda huo huo Osman  alipiga simu kama vile alikuwa akijuwa nilikuwa nikimuwaza,  niliiacha iite kidogo kisha niliipokea huku yule Muuza duka  akinitazama tu 

“Hello Osman” Nilimsalimia Osman mara baada ya kuwa  nimeshapokea simu na kusikia sauti yake 

“Jacklin, leo sijisikii vizuri naomba usimamie kazi zako  vizuri” Alisema Osman, ni kweli hata sauti yake haikuwa na  uchangamfu 

“Una shida gani Osman?” Nilimuuliza 

“Nahisi hali ya Homa tuu Jacklin” Alisema tena Osman 

“Haya nitafanya hivyo lakini baadaye….” Nilitaka kumwambia  kuwa nahitaji kuonana naye ila nilisita nikamwambia 

“Ugua pole Osman” Nilisema kisha simu ilikatika, nilirudi  kulipia ua lile kisha niliondoka nalo hadi kazini. 

Mdada wa mapokezi aliponiona alinisimamisha, alinifuata  niliposimama akaniuliza 

“Umempa nini Bosi Osman? Yaani alivyo mkali yule lakini jana  alinywea kabisa, aliposikia haupo naye aliondoka na  alionekana hana raha” Alisema, dakika moja tu ilitosha  kumtambua alikuwa ni Mtu wa aina gani, alionekana kuwa  mshakunaku, nilitabasamu kisha nikamwambia 

“Kazi njema” nilimuacha akiwa ameduwaa, pengine alitegemea  ningemwambua Mimi ni Mwanamke wa Osman nahisi ndicho  alichokuwa anataka kukisikia. 

Niliketi kwenye kiti, nilishusha pumzi zangu, niliona jinsi  maisha yangu yalivyobadilika. Mara simu yangu iliita,  aliyekuwa akinipigia alikuwa ni Mosses, aliniambia kuwa  amepata nyumba hivyo ilikuwa ikihitaji pesa kiasi cha Milioni  14, nilimwambia jioni nitampatia pesa hiyo. 

Siku hiyo, Osman alienda Hospitalini kuangalia afya yake,  alienda kwenye Hospitali ya Dokta Simon, Wawili hawa walikuwa  wakifahamiana sana. Alipofika Dokta Simon alimfanyia  uchunguzi, kwakuwa alikuwa akimfahamu vizuri Osman alijuwa ni  kitu gani kilikuwa kikimsumbua Osman, waliketi baada ya  vipimo 

“Osman! Nilikuonya kuhusu kutoa figo yako hukutaka kunisikia”  Alisema Dokta Simon, Osman alikaa kimya kumsikiliza Dokta  Simon 

“Nilikataa usifanye vile sababu ya tatizo lako, figo moja  ilikuwa na matatizo hivyo ulikuwa ukitumia zaidi figo moja  tuu, sasa ile nzima umeiondoa hii iliyobakia inafanya kazi  kwa kiwango kidogo sana na haitokuwa na muda mrefu nayo  itakufa” Alisema Dokta Simon 

“Kwanini umeamua kuhatarisha Maisha yako Osman? Wewe ni  Bilionea mkubwa hapa Nchini, una pesa ya kutosha,  unaheshimika kila kona” Aliendelea kusema Dokta Simon 

“Nilifanya vile kwasababu ya upendo wangu kwa Jacklin,  nilikuwa na Maisha yaliyojaa huzuni sana baada ya Zahra  kunitenda vibaya, ghafla sura yangu ilijawa tabasamu mara  baada ya kumuona Jacklin, niliapa sitopenda tena ila baada ya  Jacklin kuja katika Maisha yangu nimejihisi tofauti kabisa”  Alisema Osman kisha alishusha pumzi zake 

“Kwa mara ya kwanza namuona Bilionea dhahifu zaidi katika  Maisha yangu, unahatarisha Maisha yako kwa ajili ya Mwanamke  ambaye unajuwa fika ana Mwanaume wake? Unahatarisha Maisha  kwa ajili ya Mwanamke ambaye hata hujawahi kumtamkia  chochote? Hiyo ni akili yako Osman?? Laiti kama Mzee Dhabi  akilijuwa hili ulilofanya ataipoteza familia ya Jacklin na  haitokuja ionekane tena, wewe ni Mtoto wa pekee wa yule Mzee,  siku akiligundua hili anaweza hata akaniuwa Mimi” Alisema  Dokta Simon 

“Sikia Dokta Simon, naomba hili jambo liwe siri Baina yetu.  Baba yangu asijuwe chochote wakati ambao tunatafuta Figo kwa  ajili ya kunipandikiza” Alisema Osman 

“Naweza kulificha lakini hali yako inaweza ikaniumbua mbele  ya Baba yako, vyote nitafanya lakini vipi kama Jacklin  akazikataa hisia zako huoni kama utakuwa umekula hasara wewe?” Alimuuliza swali gumu sana, Osman alikunbuka namna  tukivyogombana kule Dubai, aliona Swali la Dokta Simon  lilikuwa na mashiko sana. 

Nini Kitaendelea? Usikose Sehemu Ya SITA Ya PUMZI YA MWISHO

Mpe Nguvu ADMIN Kwa ajili ya bando Kwa kumtumia Chochote aendelee kupost RIWAYA Mpya Hapa Kijiweni

Lipa Namba: 57900454
Jina: LIPA KIJIWENI TIPS
Mtandao: VODACOM  

SOMA RIWAYA YA KOTI JEUSI KWA KUBONYEZA HAPA 

SOMA RIWAYA YA FUNGATE KWA KUBONYEZA HAPA 

SOMA RIWAYA YA NILIPANGA NYUMBA MOJA NA MAJINI 

SOMA RIWAYA YA GORYANAH HAPA 

SOMA KISASI CHANGU HAPA  

SOMA RIWAYA YA MSALA HAPA

JIUNGE NIPO KIJIWENI Kwa Kubonyeza Hapa

 

Pumzi Ya Mwisho xx Pumzi Ya Mwisho xx  Pumzi Ya Mwisho xx Pumzi Ya Mwisho xx Pumzi Ya Mwisho xx Pumzi Ya Mwisho xx Pumzi Ya Mwisho xx Pumzi Ya Mwisho xx 

 

7 Comments

Leave A Reply


Exit mobile version