Ilipoishia “Nilipoanza kuhisi muda unakwenda na hakuna mtu aliyetoka, nikampa dakika tatu kwamba lazima atakuwa anavaa ndiyo maana anachelewa:

“Labda alikuwa anajisaidia haja kubwa, maana wengine huwa wanavua nguo zote, lakini mimi nipo, siendi kokote,” nilisema moyoni nikiwa bado nimesimama mlangoni kwangu.

Baada ya muda, nikasikia watu wakiongea chumbani kwao, nikashtuka, nilijikuta nikisema:

“Haa!”

Haraka sana nilitupa macho mlangoni kuangalia kandambili, nikazikuta pea mbili, nikashangaa: ”

ENDELEA SEHEMU YA NNE 

 

“Ina maana amenipita hapahapa au? Haiwezekani, asingeweza kunipita hata kama ingekuwaje?” niliwaza. Nilitoka kuelekea chooni, nikakuta mlango uko wazi, nikachungulia ndani, hakukuwa na mtu, nikanyoosha mikoni, nikarudi ndani.

Nilifikia kwenye kochi sebuleni, nikahema kwa nguvu kwani niliamini nimo ndani ya miujiza mikubwa ya ndani ya nyumba ile.

“Hivi ni kwa nini dalali alinidanganya hivi?” nilijiuliza mwenyewe nikiamini kwamba, dalali aliyenipangisha nyumba ile alijua mchezo mzima ila alitaka kupata fedha tu ndiyo maana alinipangisha bila kunipa tahadhari.

Nilitoka sebuleni, nikaenda chumbani, kitandani nikakuta ‘toilet paper’ ikiwa imekatwa sehemu. Mimi niliicha pembeni ya dirisha, lakini ikaonesha kuna mtu aliichukua na kunyofoa kidogo kisha badala ya kuirudishia palepale, yeye aliiacha kitandani.

Mbali na ‘toilet paper’ pia kuna kikopo chenye vijiti vyenye pamba za masikio kilikuwa kwenye stuli jirani na kitanda, lakini kwa muda huo kilikuwa kimeanguka chini halafu vijiti vimebaki kama vitatu tu kwa maana kwamba, aliyeingia kuchukua ‘toilet paper’ ndiye huyohuyo aliyechota vijiti vya pamba.

Nilianza kuhisi kuwa sikuwa kwenye nyumba salama, lakini kwa uthibitisho upi? Moyoni nikasema nitajua tu, mimi ndiyo mimi.

Nilikaa ndani kwangu hadi usiku ulipoingia, nikasema nibadili nguo kwa kuvaa bukta na singilendi halafu nitoke kwenda kula gengeni kwani siku hiyo sikuwa najisikia kupika chochote. Ni mara nyingi nilipenda kula gengeni.

Nilitoka, nikasimama mlangoni ili nifunge mlango wa chumbani, nilipoangalia chini, upande wa wenzangu nilikuta nje ya mlango wao pana vijiti vya pamba za masikioni vikiwa vimetumika, nikiwa katika mshango, mbele nikaona tishu ikiwa imefutiwa majimaji yenye rangi nyekundu kama damu.

Nilitembea kwa wasiwasi, nikatoka nje, sikufunga mlango kwa funguo, lakini niliubamiza tu, funguo nilikuwa nazo, nikaenda gengeni kula.

Pale kwenye genge ambapo si mbali sana na nyumbani, alikuja yule mama aliyeniuliza mimi ni mtu wa wapi, nilimsalimia, lakini kabla hajaitikia alishtuka kuniona.

“Upo kijana wangu?”

“Nipo mama, nimetoka kazini nimekuja kupata kidogo.”

“Pole sana, uoe sasa.”

“Huo ndiyo mpango wangu mama.”

“Ee, uoe halafu mimi nitakupa vyumba viwili pale kwangu, nakuahidi.”

“Nashukuru sana mama. Naanza kujipanga.”

“Sawa, vipi wenzako lakini?”

Nilisita kumjibu, nikabaki namwangalia tu, naye alibaini kwamba nimepata mshtuko na swali lake.

“Vipi wapangaji wenzako, naamini utakuwa hujaonana nao?”/

“Ni kweli mama, tena hebu nakuomba kidogo,” nilisema nikienda pembeni kidogo ili na yeye anifuate tukaongee.

“Niambie,” alianza kusema.

Nilimuuliza kama kuna anachokijua chochote kile kuhusu wale wapangaji wenzangu. Alianza kwa kusema:

“Kusema ule ukweli sina kwa undani, ila napenda kukwambia kwamba, unaishi na watu ambao unahitajika moyo wa ziada ili uweze kuendelea kuishi nao.

“Pale mbali na wewe, pameshakaa wapangaji wengine saba, tena wote kama wewe, hawajaoa. Lakini kinachoshangaza ni kwamba, wanaondoka baada ya wiki mbili, mmoja aliondoka baada ya siku tatu tu.”

“Kwa hiyo hakuna hata mmoja aliyewahi kukwambia ameona nini kule ndani?”

“Hakuna.”

“Lo! Mimi mama mambo ninayoyaona yanatisha.”

“Kama mambo yapi, nisimulie kidogo.”

Nilipotaka kuanza kumsimulia huyu mwanamke, ghafla alitokea msichana mmoja, mweupe, mrefu kiasi, amejazia sehemu mbalimbali za mwili, akaguna na kusema:

“Kaka Humuli mambo vipi, za siku?”

Nilipata kigugumizi kikubwa kumjibu mambo poa kwani sikumjua na sikuwa nakumbuka chochote kuhusu yeye, sura yake ilikataa kichwani mwangu.

“Wewe ni nani kwani?” nilimuuliza.

Akaachia tabasamu kwa mbali, uzuri wake ukaongezeka.

“Ha! Humuli, hunikumbuki mimi, kweli?”

“Sikukumbuki hata kidogo.”

“Sasa we binti, kama wewe ndiyo unamkumbuka si umkumbushe mlionana wapi?” yule mwanamke alisema kwa sauti ya mshangao.

Lakini yule msichana mrembo alimwangalia yule mwanamke kwa macho yaliyojaa hasira…

“Mama uhusiki.”

“Najua, lakini unapoteza muda kwa kuzungushazungusha wakati kumbe wewe unamkumbuka, yeye umeshajua hakukumbuki na amekwambia tayari.”

Nilishangaa kumwona yule msichana akibetua kichwa kama aliyekuwa akiweka vizuri nywele zake, ghafla yule mwanamke niliyekuwa naye akajishika kichwa na kulalamika kinamuuma sana.

“Jamani kichwa! Kichwa jamani, daa!”

“Vipi mama, imekuwaje kwani?” nilimuuliza.

“Kichwa Humuli, kinavuta ghafla! Uwiii.”

Nilianza kuogopa, nilihisi naangukiwa na msala maana akifa pale na watu waliona nikienda naye pembeni si nitahojiwa mimi?

“Kwani mama una kawaida ya kuumwa kichwa?” nilimuuliza nikimsogelea ambapo yeye sasa alikuwa ameinama.

“Sina, ndiyo nashangaa hapa.”

Niliona hakuna dawa nyingine zaidi ya kumpeleka kwake ili nikaungane na familia yake kumpeleka hospitali. Lakini kabla ya kufanya hivyo niliinua macho ili nimwambie yule dada anisaidie na kama anataka kunikumbusha, hayo yangefanyika baadaye.

Ile naanaza kusema anti huku nikiwa nimeinua macho, nilishangaa kutomwona yule msichana pale.

“Khaa!” nilijikuta nikisema hivyo.

“Mama twende nyumbani ili tukupeleke hospitali na watoto wako.”

“Ha! Mbona kimeachia,” alisema akionekana kushangaa na kuniangalia, alikuwa amepanua kinywa.

“Kweli?”

“Eee, niko mzima kabisa.”

“Au?” nilitaka kusema neno lakini zikulimaliza, nikahisi ulimi unakuwa mzito si kwa kushikwa bali kwa matakwa yangu.

“Humuli.”

“Naam.”

“Ni kweli yule binti humjui?”

“Simjui mama.”

“Kuna mawili hapo, humjui au humkumbuki.”

“Vyote mama, simkumbuki na pia simjui.”

“Lakini wewe si alikutaja kwa jina?”

“Mwenyewe nilishangaa sana.”

“Basi Humuli nimeshaelewa, kwaheri, nimeelawa ni kwa nini nimeugua kichwa na yule ni nani, pole sana wewe kijana,” alisema yule mwanamke huku akiondoka zake kuelekea kwake.

Nilimtazama, lakini baadaye nilirudi kwenye kibanda cha chipsi.

“Mzee nakuona na miss jini,” muuza chipsi mmoja alisema.

“Yupi, yule mwanamke?”

“Hapana, yule msichana.”

“Mi simjui, kwani anaishi wapi? Maana kasema ananijua, ameniita na jina.”

 “Khaa! Kumbe wewe kama sisi. Huyu dada anaishi mitaa hiihii, lakini hakuna hata mmoja anayejua nyumba anayoishi!

“Kuna jamaa mmoja anaitwa Maleke, Maleke aliwahi kumfuatilia kwa nyuma lakini alishindwa kujua aliingia nyumba gani!”

“Mh! Au jini?” niliuliza kwa mshtuko mkubwa.

Nini Kitaendelea? Usikose Sehemu Ya Tano 

SOMA RIWAYA YA KOTI JEUSI KWA KUBONYEZA HAPA 

SOMA RIWAYA YA FUNGATE KWA KUBONYEZA HAPA 

Una Enjoy Nyumba Ya Majini? Mtumie ADMIN Ahsante

Lipa Namba: 57900454
Jina: LIPA KIJIWENI TIPS
Mtandao: VODACOM 

Wewe Ni Mwandishi? Unapenda kuendeleza Taaluma yako ya uchambuzi kwenye masuala ya michezo? Mtandao wa uchambuzi wa michezo kijiweni.co.tz unakupa uwanja wa kuendeleza kipaji chako na kufikia maelfu ya wapenzi wa michezo Tanzania na nje ya Tanzania.

Tutumie makala au uchambuzi wa michezo katika barua pepe hii editor@kijiweni.co.tz  

16 Comments

  1. Official DG on

    Admini nakubali kazi zako lakini napenda kukwambia hili igizo lisha igizwa na kurushwa sinema zetu… Ila kazi iendelee

Leave A Reply


Exit mobile version