Waswahili tunasema Soka na Waingreza nao hivyo hivyo, tofauti ni hetufi tu. Soka au kwa lugha nyingine mpira wa miguu ni burudani ambayo ina watu wengi sana duniani. Wapo walioamu kuwekeza katika soka tangu zamani na hata sasa wapo wengine wenye nia hiyo. Usishangae miaka kadhaa ikayo kuiona WASAFI FC! Ni nia tu.

Soka limeajiri watu wengi, moja kwa moja na si moja kwa moja. Walioajiriwa na soka moja kwa moja ni wachezaji na walimu wao. Walioajiriwa na soka kwa njia ambayo si moja kwa moja ni kama vile waandishi wa habari za michezo, mawakala wa wachezaji, wenye mabanda ya kuonyesha mpira, wenye ving’amuzi na kadha wa kadha. Yote ni heri.

Soka hupatanisha watu, hugombanisha watu, hufurahisha watu, huhuzunisha watu, huliza watu, hudumisha amani, huleta utani wa jadi kwa mfano Simba na Yanga, huburudisha, husafirisha watu katika maeneo mbalimbali duniani, hufanya watu kufahamiana vema, huingizia watu fedha na kadhalika. Soka jilo jamani. Soka na watu, watu na soka.

Zipo timu nyingi duniani ambazo hujihusisha na soka. Kuna Kobe FC, Kumamoto FC, Enyimba, Zamalek, Mamelodi, Yanga, Simba, KRC Genk, Ajax, Liverpool, Everton, Manchester (Jiji na Muungano), PSG, KMC, BVB, Chipukizi, Maji Maji, Arusha United, Fulham, Chelsea, Arsenal, Madrid (Real na wacheza mieleka), Barcelona, Haleluya FC na nyingine nyingi. Soka huimarisha afya. Soka ni afya. Na bado zinazaliwa timu nyingine nyingi.

Kuzaliwa timu ni habari inayopendwa na wengi sasa kwani soka ni ushindani, na ushindani unahitaji watu washindane. Siyo kabla mechi hsijaanza refa anatoa penati kwa timu fulani. Hiki ni kioja vha soka. Soka ni ushindani. Na ushindani uwe wa uhalali ila si kupanga matokeo.

Katika kuzaliwa kwa timu leo tutaona namna timu ya Liverpool ilivyozaliwa, walao kwa ufupi.

Mwaka 1878 kiliundwa kikosi cha timu ya kanisa la Anglikana (Methodist New Connexion Chapel) mjini Liverpool katika kijiji cha Everton nchini Uingreza. Kanisa hilo lilikuwa na wanafunzi wake ambao walipaswa kushiriki michezo. Ili kuepusha usumbufu wa kwenda eneo jingine, basi ikaundwa timu iliyoitwa ST. Domingo Football Club.

Wakati ST. Domingo ikianzishwa, tayari kulishakuwepo na timu nyingine ambayo nayo ilikuwa chini ya kanisa. ST. Domingo FC ilikuwa kama tawi kwa ajili ya wanafunzi. Timu iliyokuwepo awali iliitwa Everton FC mali ya kanisa. Mechi ya kwanza kati ya ST. Domingo na Everton FC illisha kwa St. Domingo kuibuka na ushindi wa goli moja.

Timu hizo mbili zilikuwa haziruhusu kuchangamana wachezaji. Yaani ST. Domingo FC na Everton FC (mama) hazikuruhusu watu ambao si waumini wa kanisa lao kuja kushiriki mechi. Kutazama ni ruksa ila kucheza ni wanakanisa tu! Ni kama kuwa na timu ambayo inasimamiwa kidini na wachezaji wake wawe wa dini husika tu!

Watu walichukizwa na sheria hiyo ya kwamba asiye muumini wa kanisa hilo asicheze. Wakapaza sauti zao kwamba nao wao wana usongo wa kusakata kabumbu. Kilio chao kikasikika. Kisha Novemba 1879 uongozi wa kanisa hilo ukaziunganisha timu za ST. Domingo Everton kuwa timu moja ambayo iliichukua jina la EVERTON FC. Ndiyo hii Everton FC ya sasa!

Baada ya kuunganishwa kwa timu hizo na kuwa moja ndipo sheria ya katazo la wachezaji wasio na ushirika na kanisa hilo likaondolewa na kuruhusu watu wachangamane. Timu ikasonga mbele kwa jina la Everton FC na kanisa lake kama kawaida, lakini tu kucheza ni watu wote. Yaani watu waliokuwa wakiishi kijijini hapo bila kujali dini zao.

Tajiri mmoja aliyejulikana kwa jina la John Houlding alikuwa shabiki wa timu hiyo mpya ya Everton FC. Bwana John Houlding alikuwa mfanyabiashara na mzaliwa wa mji wa Liverpool. Kichwani mwake alifikiria kuunda tena timu nyingine ambayo itajumuisha watu wa maeneo yote ya Liverpool na si Everton pekee. Aliitunza siri hii mpaka wakati ulipofika.

Kwa kuwa John Houlding alikuwa akijihusisha pia na siasa, akaamua kuingia katika kinyang’anyiro cha uchaguzi ambao ulihitaji kupatikana kwa Meya wa Jiji la Liverpool. John Houlding akagombea na akashinda. Akawa Meya rasmi.

Akiwa Meya, John Houlding hakukata tamaa ya nia yake ya kuunda timu nyingine. Hivyo akaitisha mkutano kati yake na uongozi wa timu ya Everton ili wajadiliane uwezekano wa kuwa na timu nyingine jijini hapo. Baada ya mkutano walikubaliana kuwepo kwa timu nyingine ili kuongeza ushindani katika soka.

Hayawi hayawi, yakawa! Timu ikaundwa na kuitwa EVERTON ATHLETICS. John Houlding kwa hiyari yake akaruhusu eneo lake ambalo lilikuwa likiitwa Anfield na ndipo alipokuwa akiishi ili liwe mali ya timu kwa shughuli zote za timu. Timu hii EVERTON ATHLETICS ilijumuisha watu wote wa jiji la Liverpool. Walicheza mpira wa miguu, cricket, na mingineyo. Soka likachukua sura nyingine na likasonga mbele.

Baadae timu ya EVERTON ATHLETICS ikatambulika rasmi kama timu inayohusika na mpira wa miguu pekee na ikapewa jina jipya ambalo ni LIVERPOOL FOOTBALL CLUB. Kwenye nembo ya Everton hapa chini inaonyesha ilianza mwaka 1878, ni sawa tu. Lakini kuwa Everton pekee rasmi ni 1879 baada ya kuungana na ST. Domingo ambayo nayo ilianza 1878. Hivyo zote mbili zilianzishwa 1878 na ziliungana 1879 na kuchukua jina la Everton FC, kisha ikahesabiwa kuanza 1878. Ni kama ilivyo Tanganyika na Zanzibar. Jina ni Tanzania lakini tarehe 9 Disemba ni kumbukumbu ya uhuru wa Tanganyika ambapo jina linabaki tu Tanzania.

Muungano wa ST. Domingo FC na Everton FC (mama) ambszo zote zilikuwa mali ya kanisa ulizaa timu ya EVERTON ambayo ilitoa fursa kwa wakaazi wa Everton bila dini zao. Ikaendelea na kuwa Everton FC mpaka sasa. Ili kuongeza ushindani, Everton FC baada ya kuungana ST. Domingo FC ikazaliwa EVERTON ATHLETICS. Everton Athletics ikabadilishwa jina na kuwa LIVERPOOL FC. Basi Liverpool FC imezaliwa kutokana na ST. Domingo FC na Everton FC (mama).

Kwa hiyo Liverpool FC ni inahesabika kuwa ni timu ya Meya John Houlding hasa baada ya kujitolea eneo lake la Anfield litumike kwa ajili ya shughuli za timu. Moyo wa kujitolea huleta matunda mengi mazuri lakini usijilazimishe kujitolea kama huna nia au hauko tayari kujitolea.

Kila la kheri Liverpool na watu wake.

SOMA PIA : Hoyeee Sio Kiitikio Cha Kisoka , Siasa Iacheni Kwenye Siasa

5 Comments

  1. Jackson Kulanga on

    Exactly hii ndio Historia ya Liverpool…Lakini Kuna kitu kimerukwa cha Kujazia… John Houlding hadi anaanzisha Liverpool..ilikua ni baada ya Mgongano wa kiuendeshaji ambao watu wa Everton waliona kama Kua na Timu Mpya itaimaliza Nguvu timu yao..na kwa kua Houlding alishakua ni tajiri na Meya wakahitilafiana wakajitoa na Timu yao na Kumuacha John Houlding na Uwanja Mtupu wa Anfield.. wakapeleka Maombi ya kupewa eneo na John Houlding hakua mchoyo,yeye na uongozi wa Mji wakawapa Everton Eneo ng’ambo ya pili ya Bustani ya Stanley(Stanley Park) ..ndio walipoanza kujenga Uwanja wa Goodson Park wanaoutumia Everton Mpaka Leo.. Kisha John Houlding akaanzisha Timu ya Liverpool..mwanzoni ikawa na ukakasi wa jina kutokana na Kuwapo kwa Timu ya Rugby iliyoitwa Liverpool..wakaanza na jina Liverpool Association.
    Baadae baada ya Kutulia ikapewa kihalali jina la Liverpool FC.. wakashiriki ligi za Conference..na baadae wakafanikiwa kupata nafasi ya Kucheza play off ya Kupanda Daraja kwenda Ligi Daraja la Kwanza(Ligi Kuu ya Sasa) ..Wakacheza na timu iliyokua inawania kutoshuka ya Newton Heath( Man Utd ya sasa) wakaifunga na Kupanda Daraja..

Leave A Reply


Exit mobile version