Ilipoishia ” Sylvia alifanikiwa kunwona Brahama kwa mara ya kwanza baada ya Mwaka mmoja wa kutokuwa na mawasiliano naye, mwili wa Sylvia ulitokwa na jasho, jinsi alivyokuwa akimpenda Brahama alijikuta akidondosha chozi, Mage aliondoka ili awaache wawili hao wapate kuzungumza, Brahama alimkumbatia Sylvia ili amtulize maana aligundua Mwanamke huyo alikuwa na furaha sana kuliko hata maelezo.”

SEHEMU YA NNE -04

“Sylvia” Aliita Brahama

“Brahama ni wewe?” Alihoji Sylvia huku chozi likiendelea kumbubujika

“Ndiyo ni Mimi, nisamehe kwa kukata mawasiliano, sikutaka uumie sababu nilienda mbali na sikujuwa kama ningerudi Tanzania” Alisema Brahama akiwa anachezea nywele za Sylvia

“Unajuwa ni jinsi gani nimekusubiria Brahama hadi nikakata tamaa?”

“Najuwa Sylvia ndiyo maana ulichaguwa kuolewa na rafiki yako, nimesikia yote, hata hivyo sikutegemea kama ningekuona tena” Alisema Brahama kisha waliachana, wote waliketi.

“Bado unanipenda Sylvia?” Aliuliza Brahama swali ambalo lilijaa mtego akiwa anatambuwa fika kuwa Sylvia anampenda sana ndiyo maana alikubali kuja kuonana naye, chozi lilikuwa likiendelea kumbubujika Sylvia ambaye alishindwa amjibu nini Brahama kwani bado moyo wake ulikuwa ukimpenda sana Mwanaume huyo.

Sylvia alifuata chozi lake lililobubujika kisha alisikia simu ikiita, haraka alifungua pochi na kuangalia ni nani aliyekuwa akimpigia

“Mungu wangu!” Alisema Sylvia baada ya kuona Robson ndiye aliyekuwa akimpigia, aliiacha iite hadi ilipokata

“Nani anakupigia?” Aliuliza Brahama huku akiwa anautazama uzuri wa Sylvia

“Ni Robson, Brahama naenda” alisema Sylvia

“Sawa ushakuwa Mke wa Mtu sasa hivi” alisema Brahama, Sylvia alinyanyuka huku akiendelea kuiangalia simu yake, aliona Missed Calls zaidi ya tatu za Robson, hofu yake ikawa huwenda

Robson atakuwa amerudi, ilikuwa hivyo hivyo Robson alikuwa amesharudi.

Alipofika nje alimpigia Robson

“Mume wangu!!” Alisema Sylvia

“Naam!!”

“Samahani kwa kutopokea simu sababu ilikuwa mbali na nilikuwa na kazi kidogo” Alisema Sylvia, Robson hakutaka Sylvia ahisi chochote kile

“Oooh nimefanikiwa kupata tiketi mbili za kurejea Dar kesho”

“Oooh pole kwa pilika”

“Sawa!! Niandalie chakula basi” Alisema Robson

“Haya ndiyo nipo Jikoni hapa” Alisema Sylvia

“Haya nakuja” Alisema Robson,,Simu ilipokatika haraka haraka Sylvia aliita Bodaboda ili arejee Hotelini, Robson alidondosha chozi, akapiga moyo konde kisha alitoka Hotelini, aliacha funguo mapokezi.

Kwasababu Sylvia alichukua pikipiki wala hakuchelewa sana aliingia Hotelini, alichukua funguo kisha aliingia kwenye Apartment yao, alifanya haraka akabadilisha nguo kisha akaenda jikoni kuandaa chakula akiamini Robson alikuwa hajarudi kumbe Robson alikuwa amesharudi,

Baada ya kutoka hapo Robson alienda kwa rafiki yake akiwa mwenye msongo wa mawazo

“Mzee unapitia jambo gani? Japo ulisema sipaswi kukuingilia sababu wewe ni Mume wa Mtu ila hauonekani kuwa sawa kabisa” Alisema Rafiki yake Robson ambaye alikuwa akiishi Mwanza

“Acha Richard, hivi Mage anaishi hapa Mwanza?” Aliuliza Robson ili apate uhakika wa kile alichokisikia

“Mage yupi?”

“Yule demu mrefu ambaye alikuwaga na Mashauzi chuo?”

“Anhaaa yule Twiga” alisema Richard kisha alicheka

“Kwanini unacheka?”

“Samahani, yule ndiyo anaishi hapa Mwanza” Alisema Richard kisha alimuuliza Robson

“Ulikuwa una shida naye?”

“Hapana, ndiyo, sijui hata nikupe jibu gani lakini usijali Ahsante” Alisema Robson kisha aliondoka hapo akimwacha Richard akiwa haelewi ni kwanini Robson alimuulizia Mage.

Robson alirejea Hotelini akionekana kuwa mwenye furaha sana, alimkuta Sylvia akiwa anapika, alisimama mlango wa jikoni akamtazama Mke wake ambaye alikuwa hana habari kama Robson alikuwa amerudi, alisogea akamkumbatia kwa nyuma

“Oooh umenishtua” Alisema Sylvia akionekana kujawa na furaha isiyo pimika

“Pole Mke wangu, unapika nini?” Aliuliza Robson

“Makange ya samaki, naamini utayafurahia. Pole kwa uchovu, basi ungeenda kupumzika wakati namalizia hapa” Alisema Sylvia

“Haya sawa kuwa Muangalifu”

“Nawe pia Baby” Alijibu Sylvia, Robson aliingia chumbani, Jinamizi la Maswali na mawazo lilirudi tena kwake.

“Ina maana Brahama yupo Tanzania?” Alijiuliza Sana Robson, aliamini kurejeaa kwa Mwanaume huyo Tanzania kunaweza kusababisha ndoa yake kuharibika, alikumbuka ahadi ambayo aliitoa kwa Sylvia kuwa endapo Brahama atarejea basi yupo tayari kumwachia Sylvia, hilo lilimuumiza sana.

Akapata wazo la kukagua simu ya Mke wake ili ajiridhishe kuwa alikuwa akiwasiliana na Brahama, aliposhika simu aligundua iliwekwa namba za siri kitu ambacho hakikuwahi kutokea kabla, akajaribu simu kubwa nayo akakuta ina namba za siri.

Alihisi moyo wake unaungua taratibu, hakupata tulizo la nafsi yake kabisa, alijilaumu kwanini alikuja Mwanza kwenye Fungate, aliamini kama asingelienda Mwanza basi Sylvia asingekutana na Mage maana alikuwa akifahamu fika kuwa Mage alikuwa na ukaribu sana na Brahama.

“Nitaipigania ndoa yangu sitajali chochote, Sylvia ni halali yangu mbele za Mungu” Alijisemea Robson huku akipanga zaidi kutaka kuujuwa ukweli kuhusu Mke wake pasipo kugundulika.

Siku iliyofuata, Robson na Sylvia walikanyaga ardhi ya Jiji lenye joto na starehe yaani Dar-es-salaam, walitumia ndege ya shirika la Air Tanzania, Sylvia alionekana kuwa mwingi wa mawazo, Robson hakutaka kumuuliza sababu alishaanza kufanya utafiti Binafsi wa kutaka kujuwa kama Brahama amesharudi Tanzania.

Maisha yaliendelea, siku moja Robson alimtafuta Mark ambaye alikuwa ni rafiki yake Mkubwa, alihitaji msaada wa kimawazo zaidi japo kuna wakati alitamani kwenda kumwona mtaalam wa masuala ya Saikolojia ili amuweke sawa lakini aliona ni bora azungumze na Mark kuhusu Sylvia, siku hiyo kulikuwa na parti ya rafiki zake Mark, Robson alimuelekeza Mark kuwa waonane mahali pengine lakini Mark alimsistiza kuwa hapo alipo hakuna shida kuna sehemu tulivu sana.

Baada ya muda wa kazi Robson alienda kuonana na Mark, aliuliza baadhi ya Watu akaoneshwa

mahali tulivu ambapo Mark alikuwepo

“Bwana harusi” aliita Mark baada ya kumuona Robson akiingia, ilikuwa ni katika hali ya utani, alitegemea Robson angeingia kwenye utani pia lakini haikuwa hivyo

“Upo sawa Rob?” Aliuliza Mark ambaye alivalia pensi na raba nyeusi

“Nipo sawa sababu bado napumua lakini kiuhalisia Kaka Mimi ni Mfu Mtu” Alisema Robson, Mark alishangaa

“Ulisema hakuna kitu kinachoweza kukupa furaha Duniani kama kufunga ndoa na Sylvia, kutokuwa sawa kunatokana na nini?” Alihoji huku Muziki kwa mbali ukiendelea kusikika

“Ni kweli Sylvia ndiye mwenye funguo ya furaha yangu lakini ndiye anaye nifanya niwe katika hali hii Mark, kwa kifupi ndoa yangu inaenda kuingia doa muda siyo mrefu” Alisema Robson

“Unamaanisha nini?”

“Nahisi Sylvia anawasiliana na Brahama”

“Unasemaje?”

“Ndiyo! Nimeligundua hili Tukiwa Fungate Mwanza, inaonesha dhahiri kuwa amerejea Tanzania”

“Mmh!! Mzee una uhakika na hilo?”

“Nimelichunguza na hisia zangu zinaniambia hivyo Mark, haikuwa kawaida lakini simu zake ameweka namba za siri kitu ambacho hakuwahi kukifanya hata tulipokuwa marafiki,

inaonesha kuna mtu wa siri anawasiliana naye, unafikiria ni nani zaidi ya Brahama?”

“Kwanini unahisi Mtu wa siri ni Brahama?”

“Kuna siku tukiwa mwanza nilimpigia wakati huo nilienda kukata tiketi, kumbe nyuma alitoka na alipopokea simu yangu pengine hakuangalia ni nani anapiga nikamsikia akisema Mage nakuja mnisubirie, niliporudi nyumbani hakuwepo, sasa nilijaribu kutafiti nikagundua Mage yule dem tuliyesoma naye

chuo anaishi Mwanza na yule dem ana ukaribu sana na Brahama”

Alielezea Robson akiwa analengwa na mchozi

“Sasa usilie Rob, cha msingi kwanza ni kuhakikisha unachokihisi lakini pili kujuwa tunafanya nini maana

tukizubaa ataitumia ile ahadi yenu kukumaliza”

“Na hilo ndilo linaloninyima Usingizi Mark, sina raha sina amani, nadondosha chozi mbele yako sababu nimefikia mahali najiona ni mfungwa wa furaha yangu” Alisema Robson, Mark alimwambia

“Hebu njoo huku utulize msongo wa mawazo” Robson alimfuata Mark, wakaingia ndani ambako palikuwa na hiyo Parti

“Unatumia kinywaji gani?” Aliuliza

“Chochote tuu”

“Haya ngoja”. Mark alienda kumchukulia Robson pombe wakatafuta mahali wakakaa wakawa wanakunywa taratibu huku wakipiga stori

“Usilifikirie hilo sana kwasbabu litapata ufumbuzi endapo tutapata uhakika thabiti kuwa Sylvia anawasiliana na Brahama”

Alisema Mark katika hali ya kumuondoa hofu Robson ambaye alikuwa mwingi wa mawazo. Siku hiyo Robson alikunywa sana pombe hadi usiku akiwa na rafiki yake Mark, alikunywa hadi alihisi matatizo yameisha.

Baadaye Sylvia alimpigia simu Robson ili kujuwa yupo wapi

“Babuuu Mkeo anapiga” Alisema Mark akiwa tungi snaa

“Mke wako ananihusu nini Mimi, wewe ndiyo Mke wako siyo Mimi”

Alijibu Robson naye akiwa tungi, vicheko vya hapa na pale viliendelea huku wakizidi kupata urabu.

 

Hadi Mishale ya saa tano usiku walikuwa hawajitambui kabisa, walisaidiwa kuondoka hapo na rafiki zake Mark. Usiku huo Robson alilala kwa Mark hadi asubuhi alipoamka na kujishangaa, alimwamsha Mark

“Ebwanaa ina maana nimelala hapa?” Alihoji Robson

“Ndiyo jana tulilewa sana Rob, sijui hata tulifikaje huku, nilishtuka Alfajiri.” Alisema Mark

“Oooh Mungu wangu sijui Sylvia nitamueleza nilikuwa wapi”

Alisema Robson akiwa amejishika kichwa chake, pale pale simu ya Robson iliita, aliyepiga alikuwa ni Baba yake Mzazi,

Mstaafu wa Jeshi ambaye alikuwa akiishi Kimara Stop Over

“Kulikoni Mzee Kibu anipigie asubuhi?” Alijiuliza huku akimuuliza Rafiki yake Mark, walikuwa kitandani wakiwa wameketi, bahati nzuri siku hiyo ilikuwa ni Jumamosi hivyo hakuwa na presha kuhusu kwenda kazini

“Hebu pokea Kaka huwezi juwa anataka kusema nini” alisema Mark, Robson alifikiria mara mbili mbili akaona ni bora aipokee simu hiyo, akabofya kitufe cha kupokelea na mara moja akaiweka sikioni ili kusikia Baba yake alikuwa anataka kusema nini.

“Shikamoo Baba” Alisalimia Robson kisha alipiga mhayo

“Ina maana ndiyo unaamka sasa hivi Robson?” Aliuliza Mzee kibu

“Ndiyo Baba….”

“Mkeo anaendeleaje?” Aliuliza

“Aaah….Baabaaa…Sylvia yupo vizuri tu” alisema Robson kwa sauti ya kujiuma uma

“Mshenzi mkubwa wewe, sikuzaa kituko Mimi nina heshima zangu Robson, kama ulijiona huwezi kumudu kuishi na Mke kwanini ulioa mapema..??” Alifoka Mzee kibu na kumshtua Robson

“Babaa..”

“Ujana hujaumaliza Robson. Hebuu njoo haraka nyumbani kwangu kabla ya kwenda popote” alisema Mzee Kibu akionesha wazi alikuwa na taarifa ya Robson kulala nje ya nyumba.

 

“Oooh jesus, nini hiki ina maana Sylvia ameenda kunishtaki kwa Baba yangu?” Alijiuliza Robson huku akimpa nafasi Mark ya kutoa mawazo yake

“Ndiyo kusema anakupenda sana, basi kama ni hivyo hachepuki nje huyo” Alisema Mark

“Hebu acha ujinga Mark, Mwanamke anaweza akabadilika dakika sifuri tu. huwenda anajitengenezea mazingira ya kunipiga tukio, kwanini leo hakupiga kabisa, jana alipiga mara tatu tuu kama ushahidi” alisema Robson huku akinyanyuka lakini alihisi kizunguzungu

Alivalia nguo zake haraka haraka kisha alimwambia Mark

“Ngoja nikamsikilize Mzee kibu, kwa jinsi alivyofoka itakuwa Sylvia amemjaza maneno sana” Robson aliondoka nyumbani kwa Mark.

Akiwa Barabarani hakuacha kujiuliza maswali mengi yaliyomzonga, akakumbuka maneno ya Mark kuwa kama Sylvia ameenda kushtaki kwa Baba yake Basi huwenda hachepuki, lakini alijikanusha mwenyewe kwa kusema”Akili ya Mwanamke hainaga msimamo thabiti”

Alikanyaga mafuta, uzuri siku hiyo hakukuwa na msongamano mkubwa wa magari, hivyo alitumia wastani wa dakika kama 55 kutoka Kurasini hadi Kimara.

Muda huu alikuwa akiegesha gari yake kwenye maegesho ya magari, aliposhuka alisimama kidogo ili kujiambia majibu ambayo atampa Baba yake, mlangoni aliona viatu vya Sylvia, haikushia hapo alihisi Pafyum ya Sylvia, ilimpa uhakika kuwa Sylvia alikuwa hapo.

Alivuta kitasa akaingia ndani, akakuta Familia ikiwa inamsubiria sebleni, alikuwepo Mama yake Robson, Baba yake na Sylvia.

“Shikamoo Mama!” Alisalimia Robson

“Marahaba!!” mama yake aliitikia

“Baba nimekuja” Alisema Robson akiwa anaketi kando ya Mke wake

“Nafikiri hakuna haja ya Sylvia kujieleza tena, harufu ya pombe inayotoka kinywani mwako ni ishara tosha kuwa simu yangu ndiyo iliyokuamsha” Alisema Baba yake Robson

“Hivi Robson unaweza ukasema ulikuwa wapi Mwanangu? Ndoa changa lakini tayari tumeshaanza kusuluhisha kweli?” Alisema Mama yake Robson

“Haina haja ya kuzungumza na huyu mshenzi kwa lugha nzuri, Robson unakumbuka ni wewe uliyesema umepata tulizo la moyo wako na unahitaji kufunga ndoa? Ulilazimishwa au kuna Mtu alikusukuma ukaoa bila ridhaa yako? Ndoa ya juzi tu tayari umeanza kulala nje?” Alisema Baba yake Robson kwa suati kali

sana, Silvia akaingilia kati

“Baba inatosha, nilikuja sababu sikutaka muone namuonea Robson, nilitaka mpate uhakika….mengine nitaongea naye…Naamini tutayamaliza” Alisema Sylvia

“Unaona jinsi ulivyopata Mke mzuri na anayejuwa nini Mama ya kuwa Mke wa Mtu? Lakini wewe ni hovyo sana Robson, hovyo kabisa” Alisema Baba yake Robson, ni wazi alichukia sana

“Baba na Mama poleni kwa usumbufu, ngoja tuwaache” Alisema Sylvia kisha alimshika mkono Robson wakatoka, walipofika kwenye gari ukimya uliendelea, hadi wanafika nyumbani kwao hakuna aliyesema na mwenzake.Robson bado alikuwa na lile wazo kuwa Sikvia anachepuka na Brahama.

“Hivi umelala wapi Robson?” Aliuliza Sylvia baada ya kuingia ndani

“Kabla sijakujibu nilikuwa wapi Sylvia nataka uniambie ni kwanini simu yako ina namba za siri anbazo Mimi sizijui” alisema Robson, hakutaka kushuka chini kabisa

“Robson tokea lini ukaanza kupekua simu yangu?” Alihoji Sylvia

“Kwasababu sikuamini Sylvia” alijibu Robson

“Oooh Nani anapaswa kutomuamini mwenzake kati yangu Mimi na wewe uliyelala nje ya nyumba bila taarifa tena unarudi unanuka pombe?”

“Sylvia usinifanye kama Mtoto mdogo, usinione mimi zezeta, najuwa kuna jambo unalonificha ila nakuapia muda siyo nrefu nitapata majibu ya hilo unalolificha” alisema Robson kisha aliingia chumbani, alimpa maswali mazito Sylvia, alijiuliza mengi akiwa amesimama lakini baadaye naye aliingia chumbani.

Doa likaingia kwenye ndoa ya Robson na Sylvia huku kila mmoja akifikiria kimpango wake, hakuna aliyetaka kujishusha sababu Sylvia alikuwa akiamini anapendwa sana na Robson hivyo hawezi kufanywa chochote wakati huo Robson akimuona Sulvia ni Msaliti, japo kulikuwa na ahadi kati yao.  Nini kiliendelea? Usikose SEHEMU YA TANO-05

Wewe Ni Mwandishi? Unapenda kuendeleza Taaluma yako ya uchambuzi kwenye masuala ya michezo? Mtandao wa uchambuzi wa michezo kijiweni.co.tz unakupa uwanja wa kuendeleza kipaji chako na kufikia maelfu ya wapenzi wa michezo Tanzania na nje ya Tanzania.

Tutumie makala au uchambuzi wa michezo katika barua pepe hii editor@kijiweni.co.tz  

Fungate Sehemu Ya Kwanza 

Fungate Sehemu Ya Pili

Fungate Sehemu Ya Tatu

23 Comments

  1. Official DG on

    Aaaaaaah admini huna baya kaka…. Mwandishi nazani katokea nje ya dunia💯💯💯💯💯💯💯💯💯💯💯💯💯💯

  2. Zeyy Tabasamu✨🥰 on

    Kwan una lengo gani na sisi wasomaji Tuumwe kisukari ama Mana sio kwa utamu wa Stor zako 🙌🥰🙏

Leave A Reply


Exit mobile version