Sina shaka kabisa kwamba barua hii itakufikia mwanamfalme Dube na najua kwamba kwa muda ambao umekaa hapa nchini ni wazi kuwa ushajua Kiswahili vizuri tu na kama utakua hujaelewa basi rafiki ako mkubwa tu Zaka Zakazi atakutafsiria nilichokiandika hapa.

Kwanza ni wazi sijashtuka kabisa baada ya kuona na kusikia kuhusu kutaka kuondoka kwako katika kikosi cha matajiri wa Chamazi klabu ya Azam Fc kwani hay ani mambo ambayo yamekua yakitokea lakini kilichonishtusha zaidi ni kipindi ambacho unataka kuondoka mbona mapema sana?

Nafahamu kuwa wewe ni mchezaji mkubwa ambaye siku zote huwaza mafanikio ya timu na yako kwa ujumla na ndio maana sishangazwi na kiwango chako cha upachikaji mabao ambapo ni wazi tangu ufike Azam yaani misimu 4 una mabao 34 hakika ulikua na mchango mkubwa tu katika kikosi cha wanalambalamba.

Nikiri kuwa ulijiunga na Azam ukiwa na hitaji kubwa la kupata makombe lakini pia na kucheza kwa mafanikio makubwa katika michuano ya kimataifa jambo ambalo kwa Azam halikua hivyo ingawa waliweza kukupa pesa na sio mataji na nasikitika kuwa tangu ufike hujawahi kuchukua ubingwa wa ligi kuu.

Kuna wakati nawaza ya kuwa au wale ambao uliwaona wakitoka hapo Chamazi na kwenda Kariakoo na mafanikio ambayo wameyapata ndio jambo ambalo linakupa nguvu zaidi ya wewe kutoka hapo? Inaweza kuwa sababu na wala sitakushangaa ukisema hivyo.

Hakuna ambaye hafahamu umuhimu wako katika mechi kubwa na kamwe hakuna timu zinazoshiriki ligi kuu ambazo haiwezi kusema haikuhitaji kwani wewe ni mshambuliaji mzuri tu ambaye pia unalijua vyema lango.

Siku zote samaki wakubwa huwa wanakula samaki wadogo na naamini kuwa huu ni muda wako kwenda kutamba katika mitaa ya Kariakoo na kucheza kimataifa na kutwaa mataji.

 

SOMA ZAIDI: Azam FC Mmetengeneza Ugonjwa Utakaosumbua Ligi Kuu

1 Comment

  1. Pingback: Dondoo Na Takwimu Zote Simba Dhidi Ya Tanzania Prisons - Kijiweni

Leave A Reply


Exit mobile version