Wakati hii leo ni rasmi kuwa hatua ya 16 bora inaanza lakini michuano ya AFCON msimu huu imekuwa ya tofauti sana na wengi ambavyo walitarajia itakuwa, na hii ni kutokana na baadhi ya mataifa makubwa kufanya vibaya kwa kushindwa kupata matokeo kwa mataifa ambayo yalionekana madogo kwao na hayana uwezo wa kuwafunga.

Hiyo imesababisha makocha kutoka mataifa hayo kufukuzwa na baadhi yao kujiuzulu wenyewe kutokana na mataifa yao kufanya vibaya na mengine yakishindwa kufuzu hatua ya 16 bora, makocha hao ni ;-

1.DJAMEL BELMADI (ALGERIA)

Kocha huyu ana umri wa miaka 47, alikuwa anafundisha kikosi cha timu ya taifa ya Algeria ambapo alianza kuinoa timu ya taifa ya Algeria mwaka 2018 na mwaka 2019 alifanikiwa kutwaa ubingwa wa AFCON nchini Misri.

AFCON ya msimu huu imekuwa mbaya kwake kwani katika michezo 3 ya makundi aliyosimamia kikosi hicho amefanikiwa kukusanya alama mbili tu akipata sare michezo 2 na kufungwa mmoja.

Djamel Belmadi alifungashiwa virago muda mfupi tu baada ya mchezo wake wa mwisho wa hatua ya makundi dhidi ya Mauritania ulipomalizika na kupoteza kwa goli 1-0 na kufanya kushika mkia kwenye kundi lao.

2.CHRIS HUGHTON (GHANA)

Kocha huyu mwenye miaka 65 akiwa na uraia wa England alianza kuinoa timu ya taifa ya Ghana mwaka 2023 akichukua mikoba ya Otto Addo. Ghana ilikuwa kundi B pamoja na Misri, Msumbiji na Cape Verde, hata hivyo kikosi chake kilikusanya alama 2 tu katika michezo 3 ya makundi na kupelekea kufukuzwa na Shirikisho la Soka Ghana na moja ya sababu ni kushindwa kufuzu hatua ya mtoano ya michuano hiyo.

3.JEAN LOUIS GASSET (IVORY COAST)

Mzaliwa wa Ufaransa na Mchezaji wa zamani akiwa na miaka 70, alianza kazi ya kuinoa timu ya taifa ya Ivory Coast mwaka 2022. Licha ya timu hiyo kufanikiwa kufuzu hatua ya 16 bora ya AFCON kama “Best Looser” ila Shirikisho la Mpira nchi humo chini ya Raisi Yacine Idriss Diallo ilimfungashia virago Kocha huyo licha ya kikosi hicho kuwa wakitandaza kandanda safi na hiyo ni kutokana na wakiamini walipaswa kufuzu vizuri zaidi ya hapo.

4.TOM SAINTFIET (GAMBIA)

Kocha huyu mwenye miaka 50 akiwa na uraia wa Ubelgiji alianza kuinoa Timu ya taifa ya Gambia mwaka 2018. Tamati ya kuinoa timu ya taifa ilo ilifikia Januari 23,2024 baada ya kufungwa goli 3-2 na kumaliza hatua ya makundi wakiwa hawajakusanya alama hata moja na kupelekea kujiuzulu kwa Kocha huyo muda mchache tu baada ya mchezo dhidi ya Cameroon kutamatika. Huyu ndiyo Kocha pekee aliyejiuzuru mwenyewe baada ya timu anayoifundisha kufanya vibaya.

5.JALEL KADRI (TUNISIA)

Ana miaka 52 akiwa na uraia wa Tunisia alianza kuifundisha timu ya taifa ya Tunisia mwaka 2022.Kushindwa kufuzu hatua ya mtoano ya michuano ya AFCON licha ya Taifa ilo kupewa nafasi kubwa ya kushinda ubingwa ikawa sababu tosha ya kujiuzulu kwa Kocha huyo.

Jalel Kadri ameiongoza michezo 3 ya makundi akifanikiwa kukusanya alama 2 sawa na Sare 2 huku akipoteza mchezo mmoja dhidi ya Namibia na kupelekea kushika mkia kwenye kundi E lililokuwa na timu za taifa za Mali, Afrika Kusini na Namibia.

6.ADEL AMROUCHE (TANZANIA)

Ni raia wa Algeria akiwa na miaka 55 tu na alianza kuinoa timu ya taifa ya Tanzania mwaka 2023.Huyu  yake ipo tofauti kwani yeye alisimamishwa na Shirikisho la Soka Tanzania baada ya kukumbwa na rungu la kufungiwa michezo 8 na Shirikisho la Soka Afrika baada ya kutoa Lugha zilizokuwa zinashiria utovu wa nidhamu kwa timu ya taifa ya Morocco.

Huyu bado hajafukuzwa ila alisimamishwa na haijulikani kama ataendelea kuinoa timu ya taifa ilo au atafungashiwa virago.

SOMA ZAIDI: Nilitegemea Haya AFCON Hatua Ya Makundi

1 Comment

  1. Pingback: Namibia Imetuonesha Umuhimu Wa Kumuamini Kocha Mzawa - Kijiweni

Leave A Reply


Exit mobile version