Ilipoishia “Mi simjui, kwani anaishi wapi? Maana kasema ananijua, ameniita na jina.”

“Khaa! Kumbe wewe kama sisi. Huyu dada anaishi mitaa hiihii, lakini hakuna hata mmoja anayejua nyumba anayoishi!

“Kuna jamaa mmoja anaitwa Maleke, Maleke aliwahi kumfuatilia kwa nyuma lakini alishindwa kujua aliingia nyumba gani!”

“Mh! Au jini?” niliuliza kwa mshtuko mkubwa.

Endelea Sasa 
 SEHEMU YA TANO

“Ndivyo watu wanavyosema, sasa alipokuja kusimama na wewe, tukawa tunabishana, wengine wanasema ni miss jini, wengine siye, lakini alipokuwa anaondoka tukagundua ni miss jini.”

Basi, tuliishia hapo, nikachukua chipsi zangu na kwenda nazo nyumbani, niliamua kwenda kulia kule.

Nilifika, nikasukuma mlango mkubwa nikazama ndani kwangu. Lakini wakati napita kwenye usawa wa chumba cha wale wenzangu nikasikia vicheko, tena vicheko kwelikweli.

Sikuwajali, nikaingia sebuleni kwangu, nikafunga mlango kwa ndani, nikaweka chipsi juu ya meza, nikaenda pembeni ya chumba ambako kuna ndoo ya maji ili nichote ya kunawa.

Wakati naanza kula nilihisi na kugundua kitu. Niligundua mabakimabaki ya chipsi na kuku juu ya meza yangu wakati ukweli ni kwamba, tangu nimehamia pale sikuwahi kula chipsi wala kuku.

“Humu ndani kuna mtu anaingia kufanya mambo yake, lini mimi nimekula chipsi na kuku humu ndani?” nilijiuliza, nikasikia kicheko kutoka kwa wenzangu.

“Haa! Haaa! Ha! Haaaa…aaaa.”

Niliinua macho kuangalia juu kwenye ‘silingbodi’ kama vile niliyekuwa nimeona kitu, akili yangu ikawaza kitu cha dakika chache nyuma, nacho ni hiki:

“Humuli.”

“Naam.”

“Ni kweli yule binti humjui?”

“Simjui mama.”

“Kuna mawili hapo, humjui au humkumbuki.”

“Vyote mama, simkumbuki na pia simjui.”

“Lakini wewe si alikutaja kwa jina?”

“Mwenyewe nilishangaa sana.”

“Basi Humuli nimeshaelewa, kwaheri, nimeelawa ni kwa nini nimeugua kichwa na yule ni nani, pole sana wewe kijana.”

Nilianza kuamini kwamba, kuna uhusiano mkubwa kati ya yule msichana na wale wapangaji wa pale ndani nilipo, inawezekana alinijua jina kwa sababu naishi nao na wana uwezo wa kujua jina la mtu kulingana na mazingira yao.

 

Pia niliwaza kwamba, kuna uwezekano mkubwa yule msichana alitokea baada ya maono yao kuniona mimi na yule mama wa jirani tukitaka kuwazungumzia wao kama wapangaji wenye maajabu hivyo hawakupenda iwe hivyo ndiyo maana msichana akaibuka na kusababisha mvurugano.

“Itakuwa kweli, ndiyo maana yule mama naye alisema ameshajua ni kwa nini aliugua kichwa ghafla, alijua yule msichana ni nani na kwa nini yeye kasikia maumivu ya ghafla vile.”

“Lakini pia kuna wale wauza chipsi, nao niliwakumbuka hasa yule mmoja aliyesema yule msichana wanamjua, anaishi mtaani, lakini hawajawahi kubaini anaishi nyumba gani na kwa mzee nani wala anajishughulisha na nini,” hayo yote niliyawaza mimi.

Nilisimama, nikachukua sabuni ya kuogea ambayo haijafunguliwa, nikaipiga chini kwenye kapeti  kwa hasira huku nikisonya, nikasema kwa sauti ya chini:

“Humu ndani naishi na majini.”

Kule chumbani nikasikia wakicheka.

“Si unaona, nimesema mimi, lazima naishi nao humu ndani, da! Najuta sana,” nilisema. Kicheko kikasikika tena, safari hii kilikuwa cha juu zaidi kuliko kile cha awali.

Moyo ulijaa mawazo, akili ilihisi uchungu wa maisha, niliwaza fedha nilizozilipa kwa ajili ya kupanga mle ndani, nikamkumbuka dalili, niligundua alichofanya ni kunitapeli na hakuna lingine wala hakuwa msaada kwangu.

“Mimi ni mwanaume, kama niliweza kupata fedha za kupanga hapa, sishindwi kupata nyingine za kupanga sehemu nyingine tena mbali na hapa,” nilisema kwa moyoni.

*

Usiku nikiwa nimelala, nilichelewa sana kupata usingizi, ghafla nikaona taswira za watu ukutani, wawili tena wakiwa wamesimama, ni mwanamke na mwanaume. Niliogopa sana, nikainua kichwa polepole kuwaangalia kwa umakini, japo kulikuwa na giza, lakini niliweza kuona vizuri lakini si kwa uwazi mkubwa kama ambavyo taa ingekuwa inawaka.

Ni kweli walikuwa watu wawili kama nilivyoona, tena weupe nikimaanisha si watu weusi. Walikuwa wakionesha vitendo vya kucheka huku wakijinyonganyonga.

Kuna wakati walitembea mpaka jirani na kitanda changu kisha wakageuza na kurudi pale ukutani. Nilipeleka mkono hadi kwenye swichi ya kitanda (bed switch), nikawasha, cha ajabu sikumwona mtu wala dalili pale ukutani.

 

Niliamka nikiwa nahema kwa kasi  kifuani, nikafungua mlango na kutoka nje ili nijifanye nakwenda chooni lengo langu lilikuwa kupata picha kwa wenzangu kukoje maana niliwashuku wao na wale walioonekana chumbani kwangu.

Kwa wenzangu niliwasikia wakikoroma kwa zamu. Nikajiuliza ina maana si wao waliokuja chumbani kwangu? Niliona ni utani wa hali ya juu.

Niliamua kurudi chumbani na kukatisha safari ya kwenda chooni, nikafunga mlango wangu kwa funguo na kupanda kitandani, nilizima taa ili nione kama yale mauzauza yatatokea tena.

Ukimya ulitawala kwa muda bila kujitokeza chochote, nikaanza kupitiwa na usingizi kwa kusinziasinzia, ghafla ukutani nikawaona tena wale watu wawili.

Safari hii walikuja hadi kitandani, wakakaa, wakasimama, wakaenda kwenye kabati, wakafungua, wakatoa mashuka na kujifunika, wakayarudisha, wakaenda nyuma ya mlango, wakatungua mashati yangu mawili, wakagawana na kuyavaa kisha wakayavua, mmoja mwanaume akaenda sehemu yenye redio, akapeleka mkono, nikajua anataka kuiwasha, lakini hakufanya hivyo.

Nilichoamua kukifanya akilini ni kuwasha taa kwa ghafla na kuwavamia na nilipanga kumvamia mwanamke nikiamini ndiye aliyekuja kule kwenye chipsi. Polepole nilipeleka mkono hadi kwenye swichi, nikawasha taa kwa ghafla huku macho yangu yakiwa kwao, lakini sikumwona hata mmoja! Kwangu haikuwa mapambano bali nilichukulia kama changamoto za maisha.

Asubuhi, niliamka nikiwa nimechoka sana, lakini kabla sijatoka kitandani nilisikia nje ya mlango kukiwa na hali ya watu kutembeatembea tena kwa kasi, niliinua shingo ili nione kama nitasikia zaidi, lakini kukawa kimya

Niliamka, nikatoka, nilikwenda sebuleni kwanza kuangalia kama kuko salama.

Nilishangaa kukuta mezani kuna mfuko wa rambo uliojaa chipsi kuku kama nilivyonunua mimi, lakini zangu nilikula, sasa zile sikujua zilitoka wapi.

Niliubeba ule mfuko nikatoka nao, nilifungua mlango mkubwa wa nje nikautupia pembeni kidogo, niliporudi, nikaenda chooni, mlango ulikuwa umefungwa kwa ndani kwani hata niliposhika kitasa na kukivuta kilikuwa kigumu.

 Hii iliashiria kwamba kuna mtu, kwa hiyo moyoni nilisema nisimame palepale nje ya mlango hadi atoke. Nilisimama eneo ambalo akitoka tu, uso kwa uso na mimi.

“Tuone leo, wao si wajanja, leo nimemnasa mmoja wao,” nilisema moyoni.

Dalili zote zilionesha kwamba mle chooni mlikuwa na mtu kwani niliweza kusikia hata kuhema kwake, mara mlio wa maji, mara alikohoa, tena kwenye kukohoa nikabaini mtu mwenyewe alikuwa ni mwanamke ndiye aliyekuwa mle.

“We kohoa mpaka utapike, lakini mimi nipo hapa mpaka utoke,” nilisema moyoni.

Nilikaa sana, ikafika mahali nikachoka, lakini moyoni nikasema siondoki hata iweje, lakini nilishtuka kitu, niligundua muda mrefu sijazisikia zile dalili kama maji au kuhema, nikafunguka akili.

“Mh! Siyo kwamba ametoka?”

Ile namalizia kusema ‘ametoka?’ nikasikia kicheko kutoka kwenye chumba chao. Vicheko vikubwa sana cha kike na kiume.

Nilirudi chumbani mwili ukinisisimka, hapo ndipo niliamini mia kwa mia kwamba, nilikuwa nadili na watu wasiokuwa wa kawaida.

 

Niliingia chumbani, nikampigia simu dalali.

“Haloo,” niliita.

“Haloo. Halooo,” nilirudia lakini sikupokelewa.

Nikiwa nimeachana na simu, mara iliita yenyewe, alikuwa ni dalali nikapokea.

“Haloo,” niliita.

“Haloo,” niliitikiwa lakini sauti haikuwa ya dalali.

“Mzima bwana?” nilisalimia.

“Tuone leo, wao si wajanja, leo nimemnasa mmoja wao.”

Ha! Nilishtuka sana, nilisikia sauti yangu mwenyewe ikisema hivyo. Ikaendelea.

“We kohoa mpaka utapike, lakini mimi nipo hapa mpaka utoke.”

Nilikata simu, nilikuwa nahema sana, mapigo ya moyo yalikuwa yakienda kwa kasi ya ajabu huku nikishindwa kuona sawasawa.

“Hii ni hatari sasa,” nilisema.

Usiku wa siku hiyo sikulala kusema kweli kwani kila nilipofikiria maisha yale sikuona sababu ya kuendelea kuishi pale. Moyoni nilisema kwamba, ni afadhali ningeishi na watu ambao ni majambazi kuliko hawa, nafuu ningepanga nyumba moja na makahaba kuliko kupanga nyumba moja na majini.

Nilichoamua, asubuhi nikifika kibaruani tu niombe ruksa kisha nianze kumsaka yule dalali na pia nitafute dalali mwingine ambaye atanitafutia vyumba kwingine na si maeneo yale tena kwani niliyaona yana nuksi.

 

Asubuhi kulikucha salama kabisa, tena usiku wa siku hiyo sikuona mauzauza wala dalili zake. Nilikwenda kuoga bila kukagua mazingira, moyoni nilisema liwalo na liwe kwa maana kwamba, wawepo wasiwepo sawa tu.

Bafuni niligundua wameshaoga kwani kulikuwa na majimaji ya muda mfupi uliopita. Nilipomaliza kuoga, nilijiandaa na kutoka. Nje nilikutana na mtu ana mkokoteni, akanisalimia.

“Za asubuhi bwana mkubwa?”

“Salama, karibu sana.”

“Asante, kuna watu fulani wanaishi humu nina shida nao.”

Aliposema hivyo nilishtuka sana, niliamini yeye ni mmoja wa wale ila amejigeuza kwa kujifanya ana shughuli za mkokoteni.

“Unawajua kwa sura?” nilimuuliza huku nikiwa na wasiwasi maana alinikazia macho.

“Siwajui.”

“Sasa una shida nao kivipi watu usiowajua kwa sura?”

Ni kwamba, kuna binti mmoja huwa wanamtuma niwaletee maji, nikifika hapa huyo binti anabeba madumu kupeleka ndani, sasa jana nilikutana na huyo binti nikamuuliza kuhusu malipo yangu ya mwezi sasa, akasema nije nifuatilie mwenyewe.”

Nilishangaa sana kusikia hivyo. Nijuavyo mimi mle ndani mna watu wawili, mwanamke na mwanaume, sasa kama kuna binti hilo lilikuwa jipya kwangu, labda lakini.

“Huyo binti naye anaishi humu au?” nilimuuliza.

“Sidhani, inaonekana kama huwa wanamtuma tu.”

“Kwa nini huamini kama anaishi humuhumu ndani? Hafanani na wao wenyewe?” hili swali niliuliza likiwa na mtego mkubwa sana, nilitaka nijue uhalisia wake.

“Siwezi kusema hafanani wakati wao siwajui kwa sura.”

Hapo ndipo nilipopataka, nilidhani atasema hafanani nao, ningejua ni walewale.

“Oke, nadhani wameondoka kwenda kazini.”

“Ah! Sasa mimi fedha zangu nitazipataje jamani?”

“Subiri wakirudi jioni.”

“Wewe utakuwepo?”

Nililishangaa swali hilo, hakuwa akinidai mimi lakini anataka niwepo?

“Unataka niwepo?”

“Ee.”

“Kwa nini?”

“Naamini utanisaidia kuzipata fedha zangu.”

“Uliwahi kuja wakagoma kukupa?”

“Siyo hivyo, ila kila nikija, nikigonga mlango huwa hawafungui.”

“Basi nitakuwepo.”

“Asante kaka. Nije saa ngapi?”

“Saa moja nitakuwa nimerudi.”

Aligeuza mkokoteni na kuondoka zake huku akisema:

“Muda huo nitakuwa nimefika kaka.”

Niliondoka kwenda kazini kuomba ruksa. Lakini wakati naondoka, mfanyakazi mwenzangu mmoja aliniuliza nakwenda wapi, nikaamua kumsimulia kwa ufupi kisa changu.

“Kha! Sasa hapo tatizo liko wapi, mbona dawa ipo rahisi sana.”

“Rahisi! Ni ipi hiyo?”

“Sikia, twende pembeni nikakusimulie,” aliniambia yule mfanyakazi mwenzangu huku akiangalia kulia na kushoto kama mabosi watatokea.

Tulikwenda kusimama pembeni ya nyumba akaanza kuniambia:

“Sikiliza, kama unaishi nyumba ya namna hiyo, unachotakiwa kufanya, kila siku asubuhi na jioni au usiku unapuliza bangi ndani ya nyumba, kama ni majini, mapepo sijui nini, utaona mambo poa kabisa.”

Sikuamini maneno hayo, nikamuuliza mara mbilimbili kama ni kweli.

Nini kitaendelea? Usikose sehemu ya 06

 

SOMA RIWAYA YA KOTI JEUSI KWA KUBONYEZA HAPA 

SOMA RIWAYA YA FUNGATE KWA KUBONYEZA HAPA 

Una Enjoy Nyumba Ya Majini? Mtumie ADMIN Ahsante

Lipa Namba: 57900454
Jina: LIPA KIJIWENI TIPS
Mtandao: VODACOM 

Wewe Ni Mwandishi? Unapenda kuendeleza Taaluma yako ya uchambuzi kwenye masuala ya michezo? Mtandao wa uchambuzi wa michezo kijiweni.co.tz unakupa uwanja wa kuendeleza kipaji chako na kufikia maelfu ya wapenzi wa michezo Tanzania na nje ya Tanzania.

Tutumie makala au uchambuzi wa michezo katika barua pepe hii editor@kijiweni.co.tz  

 

 

10 Comments

  1. Bintii kimmy on

    😅😅😅apo kwenye bangi Sasa, 🙌🙌Mtunzi leta vyomboo🔥🔥🔥mambo ni firee👌😅😅

  2. Ukute majini wenyewe Ni mateja afu,mbn Wanacheka cheka ovyo …Ngoja akawashe bangi tuone😛😛

Exit mobile version